AFYA YETU

Kwa Nini Nitunze Afya Yangu?
Weka alama ya ✔ kando ya jambo ambalo ungetaka kutimiza.
□ Kupunguza mahangaiko
□ Kuzuia hasira
□ Kujiamini zaidi
□ Kuwa mwangalifu zaidi
□ Kuwa na nguvu zaidi
□ Kuboresha ngozi yangu
□ Kupunguza uzito
KUNA mambo fulani maishani ambayo ukiwa kijana huwezi kuchagua, kama vile, wazazi wako, ndugu na dada zako, mahali unapoishi, na kadhalika. Hata hivyo, afya yako ni tofauti. Ingawa urithi huchangia mambo fulani, mara nyingi hali yako ya kimwili hutegemea maisha yako.*
Huenda ukasema, ‘Umri wangu ungali mdogo sana kuanza kuhangaikia afya yangu!’ Lakini, je, ni kweli? Hebu tazama orodha ya mambo yaliyo katika ukurasa wa 71. Ulitia alama mangapi? Amini usiamini, kuwa na afya nzuri ni muhimu ili kutimiza kila moja ya mambo hayo.
Huenda una maoni kama ya Amber mwenye umri wa miaka 17, anayesema, “Siwezi kuwa nikila chakula chenye maganda, chenye mafuta kidogo na kisicho na sukari!” Ikiwa ndivyo unavyohisi pia, usiwe na wasiwasi, afya nzuri haimaanishi kuacha kabisa kula chakula chenye sukari na kufanya mazoezi makali sana kila juma. Kwa kweli, huenda ukahitaji tu kufanya marekebisho kidogo ili uwe na afya nzuri, ujihisi vizuri, na utimize mengi. Acha tuchunguze jinsi vijana wenzako walivyofanya.
Kula Vizuri—Uwe na Afya Nzuri!
Biblia inatuhimiza tuwe na kiasi katika mazoea yetu. “Usiwe mwenye . . . kujishindilia chakula,” yasema Methali 23:20. (Contemporary English Version) Nyakati nyingine, si rahisi kufuata shauri hilo.
“Sawa na vijana wengi, mimi huwa na njaa kila wakati. Wazazi wangu husema tumbo langu ni shimo lisilo na mwisho!”—Andrew, mwenye umri wa miaka 15.
“Kwa kuwa siwezi kuelewa jinsi vyakula fulani vinavyonidhuru kwa sasa, sioni vikiwa vibaya sana hivyo.”—Danielle, mwenye umri wa miaka 19.
Je, unahitaji kujizuia zaidi kuhusiana na mazoea yako ya kula? Yafuatayo ni mambo ambayo vijana wenzako wanasema yamewasaidia.
Sikiliza tumbo lako. “Nilikuwa nikihesabu kalori,” asema Julia, mwenye umri wa miaka 19, “lakini sasa ninapoanza kuhisi nimeshiba, ninaacha kula.”
Epuka vyakula visivyo na lishe. “Nilipoacha kunywa soda,” asema Peter, mwenye umri wa miaka 21, “nilipunguza uzito wangu kwa kilo tano baada ya mwezi mmoja tu!”
Epuka mazoea mabaya ya kula. “Mimi hujaribu sana kutoongeza chakula,” asema Erin, mwenye umri wa miaka 19.
Siri ya Kufanikiwa: Usikose-kose milo! Ukifanya hivyo, utakuwa na njaa nawe huenda ukashawishika kula chakula kingi zaidi.
Ukifanya Mazoezi Zaidi Utahisi Vizuri!
Biblia inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Hata hivyo, vijana wengi hawapendi kufanya mazoezi.
“Nilipokuwa shule ya sekondari vijana wengi walishindwa na somo la mazoezi. Lilikuwa somo rahisi sana, kama vile kula chakula cha mchana!”—Richard, mwenye umri wa miaka 21.
“Wengine hufikiri, ‘Kwa nini nikimbie-kimbie jua likiwaka, nitokwe na jasho na kuchoka ilhali ninaweza kucheza mchezo wa video?’”—Ruth, mwenye umri wa miaka 22.
Wewe huhisi umechoka unapofikiria tu neno “mazoezi”? Ikiwa ndivyo, zifuatazo ni faida za kuwa na mazoea mazuri ya kufanya mazoezi.
Faida ya 1. Mazoezi huongeza uwezo wa mwili wako kujikinga na maradhi. “Sikuzote baba yangu alikuwa akiniambia, ‘Ikiwa huwezi kupata wakati wa kufanya mazoezi, basi pata wakati wa kuwa mgonjwa,’” asema Rachel, mwenye umri wa miaka 19.
Faida ya 2. Mazoezi hufanya ubongo wako utokeze kemikali zinazokutuliza. “Kukimbia hunituliza, hasa wakati nina mawazo mengi,” asema Emily, mwenye umri wa miaka 16. “Mimi huhisi nimepumzika, na hisia zimetulia.”
Faida ya 3. Mazoezi yanaweza kukufanya uwe na furaha. “Mimi hufurahia kuwa nje,” asema Ruth, mwenye umri wa miaka 22, “kwa hiyo, mazoezi yangu hutia ndani kupanda milima, kuogelea, kuteleza kwenye theluji, na kuendesha baiskeli.”
Siri ya Kufanikiwa: Tenga angalau dakika 20 mara tatu kwa juma ili ufanye mazoezi unayofurahia na yatakayokufanya utumie nguvu.
Pata Usingizi wa Kutosha—Utimize Mengi!
Biblia inasema: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Pasipo usingizi mzuri, mambo yako mengi yataporomoka!
“Nisipolala vya kutosha, siwezi kufanya mambo kwa njia nzuri! Mimi hushindwa kukazia fikira jambo lolote!”—Rachel, mwenye umri wa miaka 19.
“Inapofika saa nane mchana, mimi huwa nimechoka sana hivi kwamba ninaweza kuanza kulala nikizungumza na mtu!”—Kristine, mwenye umri wa miaka 19.
Je, unahitaji kulala zaidi? Yafuatayo ni mambo ambayo vijana wenzako wamefanya.
Epuka kuchelewa kulala. “Nimekuwa nikijaribu kulala mapema,” asema Catherine, mwenye umri wa miaka 18.
Katiza mazungumzo. “Wakati mwingine marafiki hunipigia simu au kunitumia ujumbe kwenye simu usiku sana,” anasema Richard, mwenye umri wa miaka 21, “lakini sasa nimejifunza kukatiza mazungumzo ili nilale.”
Lala na uamke saa zilezile kila siku. “Siku hizi mimi hujaribu kulala na kuamka saa zilezile kila siku,” anasema Jennifer, mwenye umri wa miaka 20.
Siri ya Kufanikiwa: Jaribu kulala kwa muda wa angalau saa nane kila siku.
Utapata faida nyingi ukichukua hatua chache tu ili kutunza afya yako. Kumbuka kwamba kuwa na afya nzuri kutafanya uonekane vizuri zaidi, uhisi vizuri, na kutimiza mengi zaidi. Tofauti na mambo mengine maishani, kuboresha hali yako ya kimwili ni mojawapo ya mambo ambayo wewe unaweza kufanya. “Afya yako,” asema Erin, mwenye umri wa miaka 19, “inategemea mtu mmoja tu—wewe.”
Huelewani na wazazi wako kuhusu mavazi? Pata kujua jinsi mnavyoweza kukubaliana!
[Maelezo ya Chini]
Tunatambua kwamba watu wengi wana matatizo ya kiafya au ulemavu ambao hawawezi kubadili. Sura hii inaweza kuwasaidia wawe na afya nzuri zaidi kulingana na hali zao.
ANDIKO MUHIMU
“Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.”—1 Timotheo 4:8.
PENDEKEZO
Tafuta mtu ambaye mtafanya mazoezi pamoja. Hilo litakusaidia kushikamana na ratiba yenu kwa kuwa hungependa kumkatisha tamaa mwenzako.
JE, WAJUA . . . ?
Mazoezi ya kimwili hufanya mwili utokeze kemikali katika ubongo ambazo zinaweza kutuliza maumivu na kufanya uwe na furaha.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Mradi ninaoweza kufikia ambao ninaweza kujiwekea kuhusu chakula ni ․․․․․
Mradi ninaoweza kufikia ambao ninaweza kujiwekea kuhusu mazoezi ni ․․․․․
Nitajitahidi kulala kwa wastani wa saa ․․․․․ kila usiku kwa mwezi mzima ujao.
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kujali afya yako kutakusaidia jinsi gani kuwa mtu mwenye uhakika maishani?
● Mbali na kuhangaikia afya yako ya kimwili, ni nini cha maana hata zaidi?—1 Timotheo 4:8.
[Blabu katika ukurasa wa 74]
“Napenda jinsi ninavyohisi baada ya kufanya mazoezi. Na ninapoanza kuonekana vizuri zaidi kwa sababu ya mazoezi, hilo hunipa motisha ya kuendelea!”—Emily
[Sanduku katika ukurasa wa 73]
“Nilibadili Maisha Yangu”
“Nilipokuwa tineja, nilikuwa mnene kupita kiasi, jambo ambalo halikunipendeza kamwe. Nilihuzunishwa sana na jinsi nilivyoonekana na kuhisi! Mara kwa mara nilijaribu kupunguza uzito wangu kwa kula vyakula maalumu, lakini muda si muda nilianza kunenepa tena. Kwa hiyo, nilipokuwa na umri wa miaka 15, niliamua imetosha. Niliamua kupunguza uzito kwa njia inayofaa—njia ambayo ningeweza kudumisha katika maisha yangu yote. Nilinunua kitabu kinachozungumzia kanuni za msingi za lishe bora na jinsi ya kufanya mazoezi, nami nikaanza kutumia habari hizo maishani mwangu. Niliazimia kwamba hata nikiteleza na kuanguka au kuvunjika moyo, sitakata tamaa. Wajua nini? Nilifaulu! Baada ya mwaka mmoja, nilipunguza kilo 27. Nimedumisha uzito huo kwa miaka miwili. Sikufikiri kamwe kwamba ningeweza kufaulu! Nafikiri sababu hasa ya kufaulu kwangu si chakula fulani maalumu, bali kwamba nilibadili maisha yangu.”—Catherine, mwenye umri wa miaka 18.

No comments:

Post a Comment