Tuesday 19 April 2016

MBINU TANO KUBWA ZA KUTAFUTA KAZI


NI NANI hupata kazi bora? Je, ni yule anayestahili zaidi? “La,” anasema Brian, mshauri wa kazi. “Mara nyingi yule anayetafuta kazi akitumia mbinu nzuri ndiye hufanikiwa.” Unaweza kutumia mbinu gani kutafuta kazi? Acheni tuzungumzie madokezo matano.
Uwe Mwenye Utaratibu
Ni rahisi kuvunjika moyo ikiwa umepoteza kazi nzuri au hujaajiriwa kwa muda fulani. Katharina, mshonaji-nguo huko Ujerumani anasema, “Nilipopoteza kazi, nilitumaini kwamba nitapata nyingine. Lakini nilishuka moyo kadiri miezi ilivyopita bila kupata kazi. Mwishowe, hata ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza kuhusu jambo hilo na rafiki zangu.”
Unawezaje kukabiliana na hisia za kukata tamaa? Kitabu Get a Job in 30 Days or Less kinasema, “Inafaa upange ratiba yako kama ‘siku ya kazi’ ya kawaida ili uanze siku ukijua unapaswa kufanya nini.” Waandishi wa kitabu hicho wanapendekeza kwamba “uweke miradi ya kila siku na uandike ulichotimiza.” Kwa kuongezea, wanasema kwamba “kila siku unapaswa kuanza kwa kuvalia kana kwamba unaenda kazini.” Kwa nini? “Kuvalia inavyofaa kutafanya uwe na uhakika zaidi hata unapozungumza kwenye simu.”
Unapaswa kuona kazi ya kutafuta kazi kuwa ndiyo kazi yako, haidhuru itakuchukua muda mrefu kadiri gani. Katharina, aliyetajwa hapo awali alifuata utaratibu huo. Anasema hivi: “Nilipata anwani na namba za simu za waajiri kutoka kwenye ofisi ya serikali ya kusaidia watu kupata kazi. Nilijibu matangazo yaliyochapishwa kwenye magazeti. Nilichunguza kitabu cha simu na kuandika orodha ya kampuni ambazo zingeweza kuwa na nafasi za kazi ambazo bado hazikuwa zimetangazwa, kisha nikawasiliana nazo. Pia niliandika habari fupi kuhusu elimu na ujuzi wangu na kuituma kwa kampuni hizo.” Baada ya kutafuta kazi akitumia utaratibu huo, Katharina alipata kazi nzuri.
Tafuta Kazi Ambazo Hazijatangazwa
Mvuvi mwenye wavu mkubwa zaidi ndiye mwenye uwezekano mkubwa wa kuvua samaki. Vivyo hivyo, kujua jinsi ya kupanua “wavu” wako kutafanya uwe na uwezekano mkubwa wa kupata kazi. Ikiwa unatafuta kazi kwa kujibu tu matangazo yaliyo kwenye magazeti au kwenye Intaneti, huenda ikawa unapitwa na kazi nyingi. Kazi nyingi hazitangazwi. Unawezaje kutafuta kazi hizo?
Mbali na kujibu matangazo kama alivyofanya Katharina, unapaswa kutenga wakati kila juma wa kupiga simu kwa kampuni ambazo unafikiri huenda zikawa na kazi unazoweza kufanya. Usingoje hadi kazi hizo zitangazwe. Meneja akikuambia kwamba hakuna kazi, mwulize ikiwa anajua kampuni zilizo na nafasi za kazi na mtu unayepaswa kuzungumza naye. Akipendekeza kampuni fulani, panga kuwasiliana na kampuni hiyo ukitaja jina la mtu aliyekutuma.
Tony aliyetajwa katika makala iliyotangulia alipata kazi kwa njia hiyo. Anaeleza hivi: “Niliwasiliana na kampuni hata ingawa hazikuwa zimetangaza nafasi za kazi. Kampuni moja ilisema kwamba haikuwa na nafasi zozote wakati huo lakini ikaniambia nijaribu tena baada ya miezi mitatu. Nilifanya hivyo na nikapata kazi.”
Primrose, mama asiye na mwenzi huko Afrika Kusini, alitumia mbinu kama hiyo. Anasema: “Nilipokuwa nikihudhuria masomo ya kutoa huduma ya kwanza, niliona jengo jipya likijengwa upande ule mwingine wa barabara na nikagundua kwamba litakuwa makao ya kuwatunzia wazee. Nilijaribu mara kadhaa kukutana na msimamizi wa makao hayo. Mwishowe aliniambia kwamba hakukuwa na nafasi za kazi wakati huo. Hata hivyo, nilirudi mara kwa mara ili kuona kama ninaweza kufanya kazi mahali hapo, hata kama ni ya kujitolea. Hatimaye, niliajiriwa kazi ya muda. Nilifanya kazi zozote nilizopewa kwa bidii. Kwa sababu hiyo, nilipata ujuzi zaidi na kupata kazi ya kudumu kwenye makao hayo.”
Pia unaweza kuwauliza marafiki wako, familia, na watu wengine wakusaidie kutafuta kazi ambazo hazijatangazwa. Hivyo ndivyo Jacobus, ofisa wa usalama huko Afrika Kusini alivyopata kazi. Anasema: “Wakati kampuni niliyokuwa nikifanyia kazi ilipofilisika, niliwajulisha marafiki na watu wa familia kwamba ninatafuta kazi. Siku moja rafiki yangu mmoja alisikia mazungumzo fulani alipokuwa katika foleni ya kulipia bidhaa zake kwenye duka kubwa. Mwanamke mmoja alikuwa akimwuliza mwenzake ikiwa anajua mtu yeyote anayetafuta kazi. Rafiki yangu aliingilia mazungumzo hayo na kumwambia kunihusu. Mipango ilifanywa na nikapata kazi hiyo.”
Uwe Mwenye Kubadilikana
Ili uongeze nafasi za kupata kazi, lazima uwe mwenye kubadilikana. Jaime, aliyetajwa katika makala iliyotangulia anasema: “Kuna uwezekano mkubwa kwamba hutapata kazi unayotarajia. Unapaswa kujifunza kuridhika na kazi isiyopatana na matarajio yako.”
Kuwa mwenye kubadilikana kunamaanisha kutochagua kazi fulani. Mfikirie Ericka, anayeishi Mexico. Ingawa alisomea kazi ya katibu mtendaji, mwanzoni hakuweza kupata kazi aliyotaka. Anasema: “Nilijifunza kukubali kazi yoyote inayofaa. Kwa kipindi fulani nilifanya kazi ya kuuza vitu dukani. Pia niliuza chapati barabarani na kusafisha nyumba. Mwishowe, nilipata kazi ambayo nilikuwa nimesomea.”
Mary, aliyetajwa katika makala inayotangulia, alipopoteza kazi yake ya ukarani, aliona umuhimu wa kubadilikana. Anaeleza: “Sikusisitiza kwamba lazima nipate kazi ileile ambayo nilikuwa nikifanya. Nilichunguza kila kazi niliyotajiwa, hata kama ilikuwa kazi ambayo watu huiona kuwa ya hali ya chini. Kwa sababu hiyo, nilifaulu kupata kazi iliyoniwezesha kuwategemeza watoto wangu wawili.”
Toa Habari Kamili Kuhusu Elimu na Ujuzi
Wale wanaotoa maombi ya kazi za usimamizi, lazima waandike na kusambaza habari kuhusu elimu na ujuzi wao. Lakini hata iwe unatafuta kazi gani, habari kamili kuhusu elimu na ujuzi ulio nao inaweza kusaidia sana. Nigel, mshauri wa kazi huko Australia, anasema: “Habari kuhusu elimu na ujuzi wako huwafahamisha waajiri juu yako na mambo ambayo umetimiza na kwa nini wanakuhitaji.”
Utaandika habari gani? Andika jina lako kamili, anwani, namba ya simu, na anwani ya barua-pepe. Taja lengo lako. Taja elimu uliyo nayo na pia mazoezi na stadi ambazo umepata zinazohusiana na kazi unayotafuta. Toa habari kamili kuhusu kazi ambazo umefanya hapo awali. Taja ulichofanya na pia miradi uliyofikia na manufaa uliyoletea kampuni uliyokuwa ukifanyia kazi. Pia taja mambo uliyofanya katika kazi yako ya awali ambayo yanafanya ustahili kazi unayotafuta. Tia ndani habari za kibinafsi zinazofafanua sifa na mapendezi yako. Kwa kuwa mahitaji ya kampuni hutofautiana, huenda ukahitaji kubadili habari unazotoa kila unapotoa maombi ya kazi.
Je, unapaswa kutoa habari kuhusu elimu na ujuzi wako ikiwa unatafuta kazi kwa mara ya kwanza? Ndiyo! Huenda umefanya mambo mengi yanayoweza kuonwa kuwa ujuzi wa kazi. Kwa mfano, je, unapenda useremala au labda kurekebisha magari makuukuu? Unaweza kutaja mambo hayo. Je, umewahi kufanya kazi yoyote ya kujitolea? Taja kazi ya kujitolea ambayo umewahi kufanya na miradi uliyofikia.—Ona sanduku “Sampuli ya Habari Kuhusu Elimu na Ujuzi kwa Wasio na Ujuzi wa Kazi.”
Usipopata nafasi ya kumwona mtu unayetazamia akuajiri, acha kadi ndogo, ikiwezekana yenye ukubwa wa sentimeta 10 kwa sentimeta 15, ambayo ina jina, anwani, namba ya simu, na anwani ya barua-pepe, kutia ndani maelezo mafupi kuhusu ustadi wako na mambo ambayo umetimiza. Ikifaa, unaweza kubandika picha yako nyuma ya kadi hiyo. Wape kadi hiyo watu ambao wanaweza kukusaidia kupata kazi na uwaombe wampe mtu yeyote wanayemjua ambaye ana kazi unayotafuta. Mwajiri akiona kadi hiyo, anaweza kukupa nafasi ya mahojiano, au labda akuajiri!
Kuandika habari kuhusu elimu na ujuzi wako kunaweza kufanya uhisi ukiwa na uhakika unapotafuta kazi. Nigel, aliyetajwa hapo awali anasema: “Kuandika habari kuhusu elimu na ujuzi wako kunaweza kukusaidia upange mawazo na miradi yako. Pia kunafanya uwe na uhakika kwa sababu kutakusaidia ujitayarishe kwa ajili ya maswali ambayo huenda ukaulizwa wakati wa mahojiano ya kazi.”—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 7.
Jitayarishie Mahojiano Vizuri
Utajitayarishaje kwa ajili ya mahojiano? Huenda ukataka kufanya utafiti kuhusu kampuni unayotaka kufanyia kazi. Kadiri unavyojua mengi kuhusu kampuni hiyo, ndivyo utakavyojieleza vizuri wakati wa mahojiano. Pia utafiti wako utakusaidia kujua ikiwa kweli kampuni hiyo ina kazi unayotaka au kama ungependa kuifanyia kazi.
Kisha, fikiria mavazi utakayovaa unapoenda kwenye mahojiano. Ikiwa kazi unayotafuta inahusisha kazi ngumu, valia mavazi safi, nadhifu, na yanayofaa kazi hiyo. Kuvalia na kujipamba kwa njia nadhifu kutamwonyesha mtu unayetazamia akuajiri kwamba unajiheshimu na hivyo yaelekea utajivunia kazi yako. Ikiwa unatazamia kufanya kazi ya ofisi, vaa mavazi ambayo huonwa kuwa yanafaa kazi hiyo mahali unapoishi. Nigel anasema: “Chagua mavazi yako muda mrefu kabla ya wakati unapopaswa kwenda kwenye mahojiano ya kazi ili usifanye mambo harakaharaka na kuwa na mkazo mwingi kabla ya mahojiano.”
Nigel pia anapendekeza ufike dakika 15 hivi kabla ya mahojiano. Bila shaka, si jambo la hekima kufika mapema sana. Lakini pia kufika ukiwa umechelewa kunaweza kuharibu mambo. Wataalamu wanasema kwamba sekunde tatu za kwanza za mahojiano ni muhimu sana. Katika sekunde hizo, yule anayekuhoji hukagua sura yako na tabia yako, mambo ambayo huamua maoni yake kukuhusu. Ukichelewa, atakuwa na maoni mabaya kukuhusu. Kumbuka kwamba hutapata nafasi nyingine ya kurekebisha maoni ambayo mtu hupata kukuhusu mara ya kwanza.
Pia, kumbuka kwamba yule anayekuhoji si adui yako. Huenda yeye pia alitoa ombi kwa ajili ya kazi yake, kwa hiyo anajua jinsi unavyohisi. Kwa kweli, huenda akawa na wasiwasi kwa kuwa labda hajazoezwa vya kutosha kuwahoji watu. Isitoshe, ikiwa yule anayekuhoji ndiye mwajiri, huenda akapata hasara kubwa akiajiri mtu asiyefaa.
Ili uanze vizuri, tabasamu na umsalimu yule anayekuhoji kwa mkono ikiwa hiyo ni desturi ya kwenu. Wakati wa mahojiano, fikiria hasa mambo ambayo mwajiri anatarajia kutoka kwako na yale unayoweza kutimiza. Nigel anasema hivi kuhusu mambo unayopaswa kuepuka: “Usisimame, kuketi au kutembea kizembe. Utulivu huonyesha kwamba mtu ana uhakika. Usizungumze sana au kwa urafiki sana, wala usitumie lugha chafu kamwe. Pia epuka kuwachambua waajiri na wafanyakazi wenzako wa awali kwa kuwa ukifanya hivyo yule anayekuhoji ataona kwamba utachambua kazi hiyo pia.”
Wataalamu wanapendekeza ufanye na kusema mambo yafuatayo wakati wa mahojiano: Mtazame yule anayekuhoji, tumia ishara za kawaida unapozungumza, na uzungumze kwa ufasaha. Jibu maswali kifupi na kwa unyoofu, na uulize maswali yanayofaa kuhusu kampuni hiyo na kazi unayotarajia kufanya. Omba kazi hiyo baada ya mahojiano ikiwa bado unaitaka. Kufanya hivyo kutaonyesha kwamba bado unataka kazi hiyo.
Ukifuata mapendekezo yaliyoonyeshwa juu, huenda ukapata kazi karibuni. Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili uidumishe?


Michael Charles Chali
0712562397

No comments:

Post a Comment