Wednesday 20 April 2016

Chanzo Kikuu Cha Wivu, Matokeo Yake Na Jinsi Ya Kuondokana Na Wivu.


Habari mpenzi msomaji wetu? Karibu katika makala yetu ya leo ambapo leo tutazungumzia kuhusiana na wivu. Wivu ni nini, ni kitu gani basi mpaka kinapelekea mtu kua na wivu, nini matokeo ya wivu na namna gani au jinsi gani ya kukabiliana na wivu. Wivu ni hali ya kuwa na mtazamo hasi juu ya kitu fulani kwa mfano unachukia au hufurahii kabisa mandeleo ya mwenzako au mtu mwingine anafurahia kuona mwenzake au jirani yake akipatwa na matatizo na wakati mwingine wako watu mpaka wanafurahia misiba ya wenzao.
  Wivu ni hisia ambayo imetawala katika jamii zetu na hisia ambayo inawaumiza watu wengi sana na kuleta athari hasi katika maisha ya mtu mmoja mpaka jamii kwa ujumla. Zifuatazo ni sababu zinazopelekea mtu kuwa na wivu nazo ni;
  1. Kujiona unastahili kuliko wengine; Kujiona wewe ndio unastahili kupata kuliko wengine hiyo inapelekea wivu ukiona mwenzako kapata mafanikio juu ya kitu Fulani unaumia kweli, unapatwa na hasira kabisa na kupata maumivu ya moyo sababu ni kujiona tu wewe ndio unastahili kupata kuliko mtu mwingine. Binadamu wote ni sawa na kila mtu ana haki ya kufanikiwa hivyo hupaswi kujiona kuwa wewe unastahili kupata zaidi kuliko mwingine na ukiwa na zana hii itakutesa sana sehemu yoyote ile ulipo ukiwa kazini kwako mwenzako akipandishwa cheo unapatawa wivu na kujiona kuwa wewe ndio unastahili kuliko wengine. Hivyo kuwa huru na furahia mafanikio ya wenzako na jifunze kupitia wenzako waliofanikiwa badala ya kuonea wivu watu. SOMA; Huyu Ndiye Mtu Anayekuzuia Kufikia Mafanikio Makubwa, Na Jinsi Ya Kumshindwa.
 
2. Kutojiamini; Kutojiamini ni hali ya kujidharau wewe mwenyewe, hali ya kutojiamini inapelekea wivu sehemu mbalimbali. Kwa mfano mfanyakazi anamuonea wivu mfanyakazi mwenzake kwa sababu ya mwenzake anafanya kazi kwa juhudi na maarifa na kuongeza thamani katika kampuni au taasisi yake. Badala ya mfanyakazi mwenzake kuiga mazuri au kujifunza mazuri kutoka kwa mwenzake anaanza kumuonea wivu. Kutojiamini inampelekea kujiona yeye hawezi kuleta mabadiliko katika kampuni au taasisi yake wakati ana kila sababu ya kuwa bora kama mwenzake hivyo basi, hali hii inampelekea mtu wa kutojiamini kuwa na wivu na mwenzake. Wapo watu wengine hawajiamini katika nyadhifa walizonazo au nafasi walizonazo na kupelekea hali ya wivu hata kudiriki kumwendea mwenzake kwa mganga ili aendelee kubaki katika nyadhifa au nafasi aliyopo. Kutojiamini, kutokubali mabadiliko yanayotokea na kutokujifunza zaidi katika taaluma yako na kufanya kazi kwa mazoea bila ubora wowote inapelekea migogoro ya wivu na madhara ya wivu ni makubwa sana katika jamii. 3. Kuishi au Kuzungukwa na Watu Hasi; Kila mtu ana uamuzi wa kuishi maisha anayotaka au aliyojichagulia hivyo kama wewe umezungukwa na watu chanya katika maisha yako uko sehemu nzuri sana ya kufikia mafanikio makubwa. Lakini kama wewe umezungukwa au unaishi na watu hasi upo sehemu mbaya na ya hatari sana. Kuzungukwa na watu hasi ni kama vile kuwa na marafiki, ndugu, majirani wenye mtazamo hasi hata kuzungukwa na watu hasi katika mitandao ya kijamii inapelekea hali ya mtu kuwa na wivu unakuta mtu ameambatana na watu hasi katika mitandao ya kijamii yeye kila siku ni kuingiza umbea, majungu, katika akili yake hali hii inapelekea kujenga dhana ya wivu. SOMA; Kama Unajibebesha Mizigo Hii Katika Maisha Yako, Sahau Kuhusu Mafanikio. Matokeo ya kuwa na wivu ni kama ifuatavyo; i. Kukosa upendo na watu wengine ii. Kutopenda kuona watu wakifurahi iii. Kuishi na nyuso za huzuni iv. Kukosa furaha v. Kupata majeraha ya moyo vi. Kuishi maisha ya chuki vii. Kuishi maisha ya kutokuwa na amani viii. Huleta mauti ix. Huleta msongo wa mawazo x. Kudhoofika kiafya, kama vile kimwili, kiakili na kiroho. Namna gani au jinsi unaweza kukabiliana na wivu? Unaweza kukabiliana na wivu kwa kutumia njia zifutazo nazo ni; i. Usijilinganishe Na Mtu Mwingine; Matatizo ya wivu huanza pale mtu unapoanza kujilinganisha na mtu mwingine. Unajidharau na kujiona maisha yako unayoishi hayana maana na kuona maisha ya mwenzako ndio bora kwa njia hii lazima itakupelekea kwenye wivu tu. Utatamani kitu ambacho hakipo ndani ya uwezo wako matokeo yake mawazo hasi ya yatakutawala na kupelekea hisia za hasira na hatimaye kuwa na wivu. Hii ni dawa namba moja ya kuepukana na wivu usijilinganishe na mtu mwingine na ishi maisha yako. SOMA; Jinsi Unavyoweza Kuwa Sumaku Ya Fedha, Njia Kumi (10) Za Kuivuta Fedha Ije Kwako Muda Wote. ii. Usimdharau Mtu Mwingine; Kila binadamu ameumbwa kwa mfano na sura ya Mungu. Hivyo basi huna haki ya kumhukumu mtu mwingine na kumdharau kulingana na rangi, jinsia, jinsi, maumbile yake na hata ulemavu wowote ule. Mwenye haki ya kuhukumu si wewe bali ni Mungu acha mara moja tabia ya kuhukumu na kudharau wengine. Kama binadamu ameumbwa kwa mfano na sura ya Mungu basi ukimdharau mtu mwenzako utakuwa umemdharau aliyemuumbwa. Hakuna aliyeandika barua ya kuomba kuzaliwa na azaliwe na namna gani bali wote tunatakiwa kujipokea kama tulivyozaliwa na wala tusiwadharau watu wengine. Makala hii imeandikwa na Michael Charles Chali ambaye ni mwanafunzi  mwandishi kutoka Chuo Cha Uandishi wa habari (Dsj), mhamasishaji na mjasiriamali,unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0712562397 au kwa barua pepe micha.connect2015@gmail.com

No comments:

Post a Comment