Wednesday 20 April 2016

Sababu Zinazofanya Watu Wengine Kuwa Waongeaji Sana Bila Kuwa Watekelezaji Wa Mipango Yao.


Ni mara nyingi katika maisha yako umewahi kusikia au kuona watu ambao ni waongeaji sana wazuri wa mipango na malengo yao. Watu hawa wanapokuwa wanaongelea mipango, mikakati na malengo yao kwa hakika ni mipango mizuri ambayo ikiwekwa kwenye vitendo ni lazima kufanikiwa kuwepo.
Lakini pamoja na kuwa na mipango hiyo mizuri ambayo huwa ina uwezo wa kuwatoa watu hao hata kwenye umaskini unaowazunguka kwa bahati mbaya sana watu hao huwa siyo watekelezaji wa mipango hiyo mizuri  hujikuta ni watu kuongea tu bila kufanya kitu chochote. Hawa ni watu ambao tunao karibu kila siku na tunawajua.
Sasa kitu cha kujiuliza kwa nini watu hawa, mara nyingi huwa ni waongeaji tu bila kutekeleza kitu chochote. Kwa kawaida huwa yapo mambo yanasababisha kwa namna moja au nyingine na kujikuta wakiwa ni watu ambao hawafanyi kitu katika maisha yao. Sababu hizo huwa ni kama zifuatazo:-
1. Kutaka kujionyesha.
Wengi wa watu hawa kwa kutaka kwao sifa, na kujiona wako juu kimaisha mwisho hujikuta  ni watu wa kuongelea sana mipango yao bila kuitekeleza. Hiyo yote huja ili wao kutaka kuonekana kuwa ni watu wa hadhi fulani kumbe sivyo ndivyo. Kwa kadri utakavyojikuta unataka kujionyesha, elewa ndivyo ambavyo utendaji wako utapungua.
Kama unataka kufanikiwa, acha tabia hii mara moja. Maisha yako yanatataka yaonekane katika uhalisia wake na sio kupanga tu bila utekelezaji. Kwa kujifunza na kulijua hili unatakiwa kubadili mwelekeo mara moja na sifa zote kuweka pembeni.
2. Kutokutaka kuwajibika.
Ni kweli hiki ni kitu ambacho kinawafanya watu hawa wawe  ni watu wa kuongea kutokana na wao kutokutaka kuwajibika. Kutokana na hili la ktokupenda kuwajibika ama kujituma hujikuta ni watu ambao wanahamishia nguvu zao nyingi kwenye kuongea badala ya kutenda. Jaribu kuwachunguza wengi utawagundua wako hivi.
Hawa huwa ni watu wanaopenda sana kuonekan ni wasomi na wanajua kila kitu. Kwa sababu ya hiyo wanakuwa ni watu ambao hawawezi kuwajibika ipasavyo na hujikita kwa kushindwa kwao kuwajibika wanakuwa ni watu wa kushindwa kufanya mambo yatakayoweza kuwaletea mabadliko katika maisha yao.

3. Wanasahau mawazo yao mapema.
Pamoja na kuwa watu hawa huwa ni mafundi sana wa kuongea juu ya ndoto zao lakini huwa ni watu wa kusashau sana kile walichokiongea. Na hii huwa inatokea kutokana na wao kutoweza kuyaandika mawazo yao muhimu. Kwa kutokuyaandika mawazo muhimu ambayo wanatakiwa kuyatekeleza ndivyo hujikuta kubaki kuwa waongeaji.
Ili uweze kusonga mbele na kubadili maisha yako ikiwa unajua wewe ni mwongeaji unalazimika sana kuandika mawazo yako muhimu. Kitendo cha kuweza kuandika mawazo muhimu kutakusaidia kukupa hamasa ya kuweza kuzidi kuendelea tofauti na unavyo ongeongea tu, mwisho wa siku utajikuta unabaki kuwa mtu wa kuongea tu.
4. Kukosa hamasa kubwa ya kusonga mbele.
Mara nyingi watu hawa pamoja na kuongea sana lakini huwa ni watu ambao wanakosa hamasa ya kusonga mbele. Kwa nini kitu hiki huwa kinatokea? Hii huwa ni kwa sababu wanakuwa ni waongeaji wao sana kiasi cha kwamba wanajikuta kushindwa kupata ule muda wa kujifunza kwa wengine mambo ya kimafanikio ambayo yanaweza kuwapa hamasa zaidi, huku wakiamini wao wanaweza.
Kutokana na kushindwa kupata muda wa kujifunza kutoka kwa wengine hamasa ya kutenda au kiutendaji kwao hupungua kidogo kidogo na mwisho wa siku hupotea kabisa. Ili kuweza watu hawa kusonga mbele na kuwa watendaji ni lazima wajifunze vitu vipya kwa wengine.
Elewa kuwa, kama utazidi kuwa mwongeaji katika mambo yako sana kuliko utendaji ndivyo unavyofanya maisha yako kuwa magumu na kuyarudisha nyuma. Ni vizuri kulielewa hilo, vinginevyo itakuwa ni ngumu sana kwako kuweza kufanikiwa katika maisha yako.
Kwa makala nyingine nzuri hakikisha unatembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio iwe ya ushindi na endelea kutembelea Official Michael Charles Journalist kwa kujifunza na kuhamasika kila siku, karibu.
 

No comments:

Post a Comment